Serikali imewatoa hofu Watanzania kuwa hakuna mgonjwa yeyote aliyehisiwa
au kuthibitika kuwa na virusi vya ugonjwa hatari wa Ebola, lakini
Tanzania iko katika hatari ya kuambukizwa ugonjwa huo kutokana na
mwingiliano wa watu.
Hayo yalisemwa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na
Watoto, Ummy Mwalimu alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu
ugonjwa wa Ebola katika nchi jirani ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo
(DRC). “Nikiri kuwa Wizara imepata taarifa kuhusu mlipuko wa ugonjwa wa
Ebola katika nchi jirani ya DRC kutoka Shirika la Afya Duniani (WHO).
“Lakini hadi sasa hakuna mtu ambaye anahisiwa au kuthibitika kuwa na
virusi vya Ebola, kutokana na kupakana na DRC, nataka kukiri kwamba tuko
hatarini kuambukizwa ugonjwa huu kutokana na mwingiliano wa watu hawa
wanaosafiri kutoka na kuingia Tanzania.” Ummy alisema hatari kwa
Tanzania inatokana na kuwepo kwa mwingiliano mkubwa wa wafanyabaishara
wanaokwenda DRC, hususani wale wanaotumia njia zisizo rasmi kwa kuvuka
Ziwa Tanganyika na mitumbwi. “Napenda kutoa tahadhari kwa wananchi wote.
Tahadhari hii ni kwa nchi nzima lakini hasa katika mikoa ambayo
inapakana na DRC, hii iko katika hatari zaidi.” Aliitaja mikoa hiyo
ambayo iko katika hatari zaidi kuwa ni Kigoma, Kagera, Mwanza, Katavi,
Rukwa na Songwe. Alisema ili kujikinga na ugonjwa wa Ebola, Wizara
imeimarisha mfumo wa ufuatiliaji wa magonjwa ya mlipuko katika mikoa
ambayo inapakana na DRC, mipakani na viwanja vya ndege vyote nchini kwa
kuweka vifaa vya kubaini joto la mtu (Themo scanner).
Alisema pia wizara imeimarisha mfumo wa ufuatiliaji wagonjwa katika
mikoa yote, kusambaza miongozo, vifaa na imeagiza makatibu tawala wa
mikoa na wakuu wa mikoa kushiriki katika kutoa taarifa inapotokea dalili
zozote. “Niwatake Waganga Wakuu wa mikoa wote lakini hasa hawa ambao
wanapakana DRC wasilale, wahakikishe kunakuwa na ufuatiliaji kwa wageni
kwa kuweka daftari, mifumo na vifaa maalumu vya kutambua,” alisema. Ummy
alisema hivi sasa kuna wodi ambayo imetengwa kwa ajili ya wagonjwa wa
Ebola, watakaobainika katika Hospitali ya Rufaa ya Temeke.
Alitumia fursa hiyo kuzitaka Hospitali za Rufaa za Mbeya, KCMC mjini
Moshi na Bugando jijini Mwanza, kutenga wodi maalumu kwa ajili ya
kuwahudumia wagonjwa wa milipuko ikiwamo Ebola. Ummy aliwataka
Watanzania kuchukua tahadhari, kwa kuepuka kugusa au kuingiwa na mate,
damu, mkojo, kinyesi, machozi na majimaji mengine yanayotoka mwilini mwa
mwenye dalili za ugonjwa wa Ebola.
Pia kuepuka kushughulikia maiti ya mtu aliyekufa na Ebola, kuzingatia
usafi wa mwili, kuwahi vituo vya afya, kutoa taarifa kwa viongozi wa
serikali katika ngazi zote. Dalili za mgonjwa huanza kuonekana kwa mtu
aliyeambukizwa baada ya siku 2 hadi 21 tangu kupata maambukizi. Dalili
hizo ni homa kali ya ghafla, kulegea mwili, maumivu ya misuli, kuumwa
kichwa na vidonda kooni.
Mara nyingi dalili hizi hufuatiwa na kutapika, kuharisha, vipele vya
ngozi na pia figo na ini kushindwa kufanya kazi. Baadhi ya wagonjwa
hutokwa na damu nyingi ndani na nje ya mwili. WHO imetoa taarifa ya
kulipuka kwa ugonjwa wa Ebola katika nchi ya DRC katika mji wa Biloko
Jimbo la Ikweta, baada ya kubainika kuwapo wagonjwa 21 na 17 kati yao
wakiwa wamepoteza maisha. Mwaka jana kulitokea mlipuko wa Ebola katika
eneo hilo, ambapo watu wanne walifariki dunia.
Chanzo:HabariLeo 11/05/2018
Saturday, May 12, 2018
SERIKALI YASISITIZA HAKUNA MGONJWA WA EBOLA
Tags
# HABARI NA MATUKIO
About Prosper
Soratemplates is a blogger resources site is a provider of high quality blogger template with premium looking layout and robust design. The main mission of templatesyard is to provide the best quality blogger templates.
HABARI NA MATUKIO
Labels:
HABARI NA MATUKIO
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment